Biashara

Deni la Sh275 bilioni lailiza Tanesco

Dar es Salaam. Shirika la Umeme (Tanesco) limesema limbikizo la deni la Sh275 bilioni kwa taasisi mbalimbali za Serikali na wateja binafsi, linachangia kukwamisha utekelezaji wa miradi mbalimbali.
Hata hivyo, Tanesco imeelezwa kuwa deni hilo limeanza kupunguzwa na mpaka kufikia Juni, mwaka huu, takriban Sh30 bilioni zilikwishalipwa na wadaiwa.
Kutokana na ukosefu wa fedha, Tanesco inafanya juhudi za ziada ili kufanyia matengenezo transfoma inayosambaza umeme katika eneo kubwa la Kipawa jijini.
Akizungumza jana na gazeti hili, msemaji wa shirika hilo, Adrian Severin alisema hutamani kufanya kazi bila kuwakera wateja wao, lakini tatizo la fedha linawafanya washindwe kufikia malengo.
Hata hivyo, Severin alisema baada ya kufikia kikomo cha muda wa tangazo la ukusanyaji wa madeni hayo, Tanesco itaanza kuchukua hatua kali dhidi ya wadaiwa wote sugu.
 “Kuna ripoti ambayo tutaipokea leo (jana) itakayokuwa na mwelekeo wa jinsi gani tutakusanya madeni hayo. Inasikitisha kuona taasisi za Serikali na wateja wengine hawalipi madeni yao wakati wanaendelea kupata huduma,” alisema.
“Shirika linaathirika sana na deni hilo, tunashindwa kutoa huduma kwa ufanisi katika maeneo mengi kwa sababu ya kukosa fedha. Kiasi hicho kama kingekuwapo kingeweza kusaidia kutatua changamoto hizi ambazo kwa kweli ni kero kubwa kwa wateja wengine.”
Akizungumzia transfoma ya Kipawa, Severin alisema mainjinia wa Tanesco wamebaini tatizo kubwa ambalo litatatuliwa baada ya siku tatu mpaka nne.
“Kuna mtaalamu atafika leo (tangu jana) kutoka India kwa ajili ya kuitengeneza. Inaweza kukamilika Jumatano au Alhamisi,” alisema alisema Severin.
Alisema kuharibika kwa transfoma hiyo, kumeyafanya maeneo ya Kisarawe, Gongo la Mboto, Kivule, Kipunguni, Ukonga, Tabata, Uwanja wa Ndege, Chang’ombe, Tandika, Nyerere Road na maeneo jirani kukosa umeme.
Alisema ili kupunguza usumbufu, umeme unaotumiwa katika makazi ya watu kwa sasa utatoka katika transfoma ya Ubungo, “lakini kwa viwanda itabidi wasubiri mpaka matengenezo yatapokamilika.”

Boti isiyotumia nahodha yavumbuliwa nchini


Dar es Salaam. Mamlaka ya Mafunzo na Ufundi Stadi (Veta) imevumbua boti inayojiendesha bila nahodha ambayo ina uwezo wa kutuma taarifa za kijasusi na kujilinda dhidi ya mashambulizi au uharibifu unaoweza kufanywa na watu wenye nia mbaya.
Akizungumza wakati wa Maonyesho ya 38 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF) katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere jijini hapa jana, Mvumbuzi wa mashine hiyo, Immanuel Bukuku alisema kuwa imemchukua miezi sita kufanikisha uundaji wa mashine hiyo.
Alisema uvumbuzi huo umeambatana na majaribio ambayo yamefanyika katika Pwani ya Kigamboni na yameonyesha mafanikio makubwa na ipo tayari kwa ajili ya matumizi ikiwa na kamera za kutosha kwa ajili ya uchunguzi na kupeleka taarifa.
“Uvumbuzi umekamilika na boti ipo tayari kwa ajili ya matumizi na wadau wanakaribishwa kwa ajili ya kusaidia ufanikishaji wa utengenezaji wa boti nyingine zaidi,” alisema na kuongeza kuwa boti hiyo itakuwa inaongozwa na mashine nyingine itakayo kuwa sehemu maalumu.
Bukuku ambaye ni mwalimu wa masuala ya Sayansi na Teknolojia katika Chuo cha Veta Chang’ombe alisema amevumbua boti hiyo ambayo imetengenezwa kwa kutumia vifaa rafiki na mazingira ya bahari na inatumia mfumo wa umeme jua na mashine za kuzalisha umeme.
“Ina uwezo wa kuhisi kuwapo kwa mtu au chombo kingine jirani yake na kutoa taarifa katika sehemu ambako kinaratibiwa, pia ina uwezo wa kushambulia kwa kutumia mitutu na ina uwezo mkubwa katika masuala ya ulinzi na usalama,” alisema.
Alisema pia amefanikiwa kutengeneza injini ya ndege ambayo imeonyesha mafanikio kwa kiasi kikubwa na wakati wowote inaweza kutumika na mafanikio hayo yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na mpango wa Veta wa kuwa na Kitengo cha Masuala ya Ufundi na Ubunifu.
“Kuna mashine na teknolojia nyingi ambazo zimevumbuliwa hapa, ni dalili njema na tuna matumaini kuwa uvumbuzi zaidi unafuata kutokana na tafiti nyingi kuonyesha dalili za mafanikio,” alisema na kuongeza kuwa kitengo hicho kimepania kubadili mwelekeo mzima wa Veta kwa hivi sasa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

KUWEKA TANGAZO LAKO HAPA NI BEI NAFUU
KUWEKA TANGAZO LAKO HAPA NI BEI NAFUU

TANGAZO LA KAZI -Commited youth agricultural organisation CYAO is looking for a person who is specialised in agriculture

POSITION DESRIPTION;

Agricultural Technician

Qualifications

Diploma in agriculture

Mode of application applicant must send an updated Cv,birth cirtificate,one recent passport size, an accademic cirtificate, age limit 20 to 35

apply to Project cordinator,Commited youth agriculture organisation,P.O.Box 78438 Dar es salaam or you can call through +255657990920/+255754823728