15 Aprili 2015

Serikali kuzifuta taasisi za kidini zinazojihusisha na Katiba,Uchaguzi mkuu

Dar es Salaam. Serikali imetishia kuanza kutekeleza sheria inayodhibiti asasi za kijamii na kidini, ikizitaka taasisi hizo kuacha mara moja kutoa matamko yanayolenga kuwashawishi waumini wao waikatae Katiba Inayopendekezwa na pia kuwapangia nini cha kufanya katika Uchaguzi Mkuu ujao na kusema watakaobainika watachukuliwa hatua kali.
Katika kuzipiga ‘kufuri’ taasisi hizo, Serikali imesema kuanzia Aprili 20 itazifuta taasisi zote zilizosajiliwa na Wizara ya Mambo ya Ndani ambazo havifuati matakwa ya kisheria ya kuwasilisha taarifa zao za mwaka za ukaguzi wa hesabu na kulipa ada za kisheria.
Hata hivyo, viongozi wa dini ya Kikristo na Kiislamu waliozungumza na gazeti hili jana kuhusu kauli hiyo, wamesema taasisi zao zinawakilisha watu, na hivyo zina haki ya kikatiba na kisheria kupinga jambo lolote zitakaloona linakwenda kinyume na maslahi ya Taifa na kwamba ziko tayari kukaguliwa.
Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe alisema jana kuwa kazi hiyo ya kupitia usajili wa vyama hivyo itaanza kwa vyama vilivyopo jijini Dar es Salaam, baadaye kuendelea nchi nzima. Vyama vyote vitakavyofutiwa usajili vitawekwa katika tovuti ya wizara hiyo na havitaruhusiwa kuendelea na shughuli zake.
“Matukio ya aina hii yanapofanyika yanaashiria kuvuruga amani na utulivu nchini. Kazi ya Serikali ni kuhakikisha usalama wa watu wote unaimarishwa ili shughuli zote za kisiasa, kidini, kijamii na kiuchumi, zinatekelezwa kwa misingi ya kisheria,” alisema Chikawe.
Uamuzi huo umekuja wakati Jukwaa la Wakristo likiwa limetoa tamko la kuwataka waumini wake kujiandikisha kwa wingi katika Daftari la Kudumu la Wapigakura, kuisoma Katiba Inayopendekezwa na kujitokeza kuikataa kwa kupiga kura ya hapana.
Jukwaa hilo, linaloundwa na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania (TEC) na Umoja wa Kanisa la Pentekoste Tanzania (CPCT), linadai kuwa Serikali imewaahidi Waislamu kuwapa Mahakama ya Kadhi ili waipigie Katiba Inayopendekezwa kura ya ndiyo. Jambo ambalo limesema litasababisha mgawanyiko.
Mbali na jukwaa hilo, pia Jumuiya na Taasisi za Kiislamu liliwataka waumini wake kuikataa Katiba Inayopendekezwa iwapo Serikali itashindwa kuwasilisha bungeni muswada wa Mahakama ya Kadhi ili chombo hicho kitambulike kisheria. Muswada huo uliondolewa baada ya kuibuka kwa mvutano mkali katika mkutano wa 19 wa Bunge uliomalizika Aprili Mosi, mwaka huu.
Katika siku za hivi karibuni viongozi mbalimbali wa dini wamekuwa wakitaja wazi sifa na hata majina ya watu wanaopaswa kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu ujao, na wakati fulani vikundi vya wachungaji na masheikh kwa nyakati tofauti vilienda nyumbani kwa kada wa CCM, Edward Lowassa mjini Dodoma kumshawishi atangaze nia ya kugombea urais.
“Kauli za viongozi wa dini kuhusu masuala ya Katiba au Uchaguzi Mkuu ujao zinakiuka sheria za usajili wa taasisi zao. Viongozi ambao tayari wameshatoa matamko ya aina hiyo tunawapa onyo kwa sasa, wasirudie tena,” alisema Waziri Chikawe.
Alisema waumini wana haki ya kuamini mafundisho ya dini zao, lakini wanapaswa kutekeleza masuala yao ya kisiasa na kijamii kwa utashi wao bila ya kushawishiwa na mtu yeyote, kama sheria za nchi zinavyotaka.
“Mfano ni pale kiongozi au viongozi wa dini wanapochangisha fedha za kuandamana au kukutana na wanasiasa kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kuwashawishi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi. Hii si kazi ya taasisi za dini na ni kinyume na sheria,” alisema.
Alisema wananchi, vikundi na taasisi za dini zinatakiwa kuepuka kushiriki katika vitendo ambavyo vinaashiria kuvuruga amani na utulivu nchini.
“Serikali itachukua hatua kali kwa watu binafsi, vyama vya siasa na taasisi za dini zitakazobainika kuvuruga usalama na utulivu wa nchi, ikiwa ni pamoja na kuvifuta katika daftari la usajili wa vyama vya kijamii ambavyo vitakiuka Katiba ya kuanzishwa kwake,” alisema.
Viongozi wa dini wajibu
Wakizungumzia kauli hiyo ya Serikali, viongozi wa dini walikosoa tamko hilo wakisema linalenga kuwafumba midomo.
“Ninachoamini, taasisi zote zipo kwa mujibu wa sheria. Kama Serikali inataka kuzibana hizi taasisi zisifanye kazi kwa uhuru wake, itunge sheria nyingine ya kuzibana, hata hizo sheria mpya tutahakikisha zinapitiwa na kujadiliwa kabla ya kupitishwa. Tupo tayari kufanyiwa ukaguzi,” alisema katibu wa CCT, Dk Leonard Mtaita. Alisema jumuiya hiyo inawakilisha watu ambao ndio inawasemea, hivyo haina hofu yoyote juu ya kuendelea kufanya kazi zake kwa uhuru na kungalia maslahi ya taifa.
Naibu katibu wa Jumuiya ya Taasisi za Kiislam na Shura ya Maimam, Rajab Katimba alisema: “Kutengeneza tishio kwa taasisi  ni kutaka kuzifumba mdomo kwa sababu Televisheni ya Taifa (TBC) inahamasisha kura ya ndiyo kuhusu Katiba, wakiwemo wabunge na viongozi wa serikali.”
Alisema hakuna dhambi yoyote iwapo taasisi mbalimbali zitawaeleza Watanzania ukweli wa yaliyomo katika Katiba Inayopendekezwa.
“Kukagua ni haki yao. Viongozi wa dini wanayo haki ya kutokubaliana na jambo lolote ambalo wataona halina maslahi kwa Taifa. Tutapinga tu haitakuwa haki kukubaliana na kitu ambacho hakina maslahi kwa Watanzania, eti tu kwa hofu ya kufungiwa,” alisema.
Naye Sheikh Khamis Mataka, ambaye ni katibu mkuu wa Taasisi ya Masheikh Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania, Sheikh alisema: “Taasisi za dini zinalea na kuwajenga kiroho waumini. Lengo la serikali wakati wote lionekane kuziimarisha na si kutengeneza mazingira ya kuzifunga mdomo.”
Wanasheria
Akizungumzia kauli hiyo, mwenyekiti wa Baraza la Katiba Zanzibar, Profesa Abdul Sheriff alisema hizo ni dalili za Serikali kuongeza petrol kwenye moto.
“Dalili zilianza kuonekana muda mrefu jinsi serikali ilivyoanza kuongeza petroli katika moto, inataka kufanya jambo la hatari kwa kuzifumba mdomo taasisi mbalimbali,” alisema Profesa Sherrif.
Alisema kufutiwa kwa usajili kwa vyama hivyo ni taratibu za kisheria na si agizo la kisiasa, na kwamba hakuna taasisi yoyote ambayo itakuwa tayari kuogopa tishio la Serikali kwa kuwa itapinga mahakamani.
Mkurugenzi mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Hellen-Kijo Bisimba  aliona tamko hilo kuwa ni woga wa Serikali.
 “Ninachokiona ni hofu na woga tu kwa sababu Serikali inajua nguvu ya taasisi katika ushawishi wake kwa wananchi. Zinaweza kukwamisha mipango ya serikali,” alisema.
Alisema Serikali inataka kuzifungia taasisi hizo wakati ikijua wazi kuwa kila raia ni sehemu ya siasa.
“Sijui wanaitafsiri vipi siasa? Ninachofahamu ni kuwa kila raia yupo ndani ya siasa? (Serikali) Inajaribu kutaka kutumia nguvu kupitisha maslahi yake,” alisema.
Waziri Chikawe alisema jijini Dar es Salaam jana kuwa onyo hilo pia linawagusa watu binafsi na vyama vya siasa vinavyobeba wanachama wake kutoka eneo moja kwenda jingine kuhudhuria mikutano ya hadhara, akisema kuwa jambo hilo ni chanzo cha vurugu na linatakiwa kuachwa mara moja.
Chikawe pia alipiga marufuku tabia ya vyama vya siasa ya kubeba wanachama kutoka eneo moja kwenda jingine kuhudhuria mikutano ya hadhara kwa maelezo kuwa hali hiyo imekuwa chanzo cha vurugu.
“Utekelezaji wa jambo hili utapunguza ushabiki wa kisiasa na pia tatizo la uvamizi wa wanachama wanapokuwa wanatoka kwenye mikutano ya mbali na maeneo hayo. Kwanza tutapunguza mzigo wa ulinzi kwa askari wetu. Huwezi kutoa watu Mbagala kuja katika mkutano Gongo la Mboto,” alisema.
Chikawe pia aligusia suala la ugaidi akisema Serikali imejipanga kukabiliana nalo, ikiwa ni pamoja na kuwafuatilia watu wote wanaoingia na kutoka nchini, huku akiwataka wazazi kuwa karibu na watoto wao ili wasijiingize katika vitendo hivyo.
“Jeshi letu ni imara sana katika nchi za Afrika Mashariki na ya Kati. Msiwe na wasiwasi tupo salama sana,” alisema.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

KUWEKA TANGAZO LAKO HAPA NI BEI NAFUU
KUWEKA TANGAZO LAKO HAPA NI BEI NAFUU

TANGAZO LA KAZI -Commited youth agricultural organisation CYAO is looking for a person who is specialised in agriculture

POSITION DESRIPTION;

Agricultural Technician

Qualifications

Diploma in agriculture

Mode of application applicant must send an updated Cv,birth cirtificate,one recent passport size, an accademic cirtificate, age limit 20 to 35

apply to Project cordinator,Commited youth agriculture organisation,P.O.Box 78438 Dar es salaam or you can call through +255657990920/+255754823728